RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

NDOA YA JOTI YAMPONZA PADRI



Mchekeshaji Lucas Lazaro Mhuvile almaarufu Joti akiwa na mke wake Tumaini akijiandaa kumvalisha pete kanisani.

DAR ES SALAAM: Wakati ndoa ya mchekeshaji Lucas Lazaro Mhuvile almaarufu Joti ikitikisa katika Jiji la Dar, wikiendi iliyopita, padri aliyefungisha ungano hilo ameingia matatani baada ya baadhi ya waumini kuhoji kiduku cha bwana harusi kanisani.

Joti, mmoja wa wachekeshaji wa Kundi la Orijino Komedi, alifunga ndoa na mchumba wake wa siku nyingi aitwaye Tumaini Salehe katika Kanisa Katoliki-Magomeni jijini Dar, Jumamosi iliyopita huku akiwa amenyoa kiduku (nywele zinazobaki katikati ya kichwa huku za pembeni zikiwa zimenyolewa), kitendo ambacho kiliwafanya baadhi ya waumini waliojazana ukumbini hapo kupigwa na butwaa. “Sasa hivi ndiyo nini tena jamani? Yaani kweli padri anaruhusu hili jambo linafanyika kanisani?

Huu si mtindo wa vijana wa kihuni wanaouonesha huko mitaani, unaruhusu hili jambo au kwa sababu huyu ni kijana maarufu?” Alihoji mama mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Mama Baby.


Licha ya Mama Baby, muumini mwingine ambaye naye alikuwepo kanisani hapo, alisema kuwa, kitendo cha kuruhusu watu kuoa wakiwa na nywele za mitindo ya kihuni kama vile siyo sawa, kwani ni rahisi kuruhusu vitu vingine visivyo vya kimaadili kufanywa na vijana hasa wa kizazi cha sasa.

Ijumaa Wikienda lilikuwepo kanisani hapo hivyo lilimfuata padri aliyefungisha ndoa hiyo, Father Paul Sabuni ili kuzungumzia shaka hiyo ya baadhi ya waumini, ambapo alisema kuwa, kiduku hakijawahi kuwa tatizo kwa Kanisa Katoliki.

“Kanisa haliangalii mavazi au namna mtu alivyo, kanisa linaangalia moyo wa mtu, kama roho yake iko safi hicho ndicho tunachokitaka, suala la kiduku halina nafasi kwetu, tunashughulika na imani yake, si muonekano wala mavazi yake, hao wanaofikiri hivyo wanapaswa kupewa somo.


“Nachukua nafasi hii kumpongeza sana Joti kwa uamuzi sahihi aliofikia, kitendo chake cha kuamua kufunga ndoa ni cha kupongezwa na kinachopaswa kuigwa na mastaa wengine.

“Kwa ustaa wake angeweza kuendelea kuishi maisha ya bila ndoa na kila kitu kingekwenda, lakini amefanya jambo la busara sana kuchukua uamuzi wa kuoa ili atulie na mkewe,” alisema padri huyo.

Vinginevyo, mamia ya watu waliohudhuria harusi hiyo walipagawa na jinsi muigizaji huyo alivyokuwa kivutio machoni mwao, kwani wengi wa waliosikia kuhusu harusi hiyo, walijua ni matangazo kama ambavyo imewahi kutokea mara kadhaa huko nyuma.

Kwa muda wote wa shughuli hiyo kanisani hapo na hata kwenye Ukumbi wa Mlimani City, watu hao walionekana kufurahia na mara kadhaa, Joti alifanya vituko vya hapa na pale katika kukoleza tukio hilo, akiwa ni memba wa pili wa kundi hilo kupata jiko, baada ya Emmanuel Mgaya ‘Masanja Mkandamizaji’ kufanya hivyo miezi kadhaa iliyopita.

Comments